Mtakatifu SIMON KITURURU - MAWAZONI

FALSAFA na WAZO ndani ya neno - DUH!

Tulijifunza nini kutoka Kwa akina Khmer Rouge na Mao Tse-Tung

>> Friday, November 24, 2006

Baadhi ya Mafuvu ya waliokufa baada ya Khmer Rouge kuamua watu wote wawe wakulima.








Nimejikuta katika siku za karibuni nikiingia katika mijadala ya kilimo. Baadhi ya watu wamekuwa wakifikiri kuwa nabisha kuwa kilimo si muhimu hasa baada ya kusema kwamba siamini kuwa matatizo ya Tanzania yana jibu moja kama baadhi ya watu wapendavyo kutaja kilimo kama ndio jawabu pekee. Mwanablogu Luihamu alifikia mpaka kutunga shairi akitaja jina langu na la Ndesanjo kuhusiana na maswala haya ya kusisitizia umuhimu wa kujali umuhimu wa nyenzo nyingine katika kutatua matatizo ya Tanzania. Bado hapa napenda kukazia kuwa tunahitaji kila ujuzi ilikuweza kufanikiwa Tanzania. Mkulima alivyo muhimu ndio hata mwana tekinolojia, mwana sayansi ya jamii, mfanyabiashara, nesi , dakitari na taaluma zote zilivyo muhimu katika kujenga nchi yetu.

Nimeona labda nikumbushe watu historia kidogo igusayo maswala yawezayo kutokea kama mkazo wa mambo ukiwa katika eneo moja liaminikalo kuwa hilo pekee ndio njia. Naamini kuwa binadamu kama angeweza kujifunza kutoka katika makosa basi kunauwezekano wakutopoteza muda katika kutafuta matatuzi mengi tu. Siamini kuwa ni lazima kila mtu apitie katika makosa hayohayo wakati unaweza kujifunza kwa makosa wengine waliofanya. Sidhani ni mpaka ushike moto iliujue unaunguza.Naamini mambo mengi tunaweza kujifunza kutokana na kutafakari mafanikio na makosa yetu na yale ya wenzetu hapa duniani. Naamini kwa kufahamu vikwazo na virahisisha mambo ambavyo twaweza kujifunza kutoka kwa wengine tunapata muda wa kuweza kukwepa kurudia makosa na kukazia miundo mbinu ituwezeshayo kuyakabili mazingira yetu na matatizo yetu. Naamini kama Watanzania tunamengi tumefanikiwa na mengi tumekosea na tunazidi kukosea. Ni kweli kama Watanzania si kweli majawabu yote au njia zote walizopita watu wengine basi nasi zitatufikisha paradiso.Ila naamini kuwa kuna mengi twaweza kujifunza kupitia machambuzi ya ni nini wenzetu walifanya na wanafanya katika kutatua matatizo yao. Mara nyingi tunakazanina kujifuza kutoka katika nchi zisemekanazo kuwa zimeendele. Mara nyingi tunasahau kuangalia nchi nyingine ,hasa hatutaki kujifunza kupitia makosa ya wengine. Ili Tanzania iendelee tunahitaji busara zitokazo kila pande na sio tu zile tu ambazo twafikiri ni za nchi zisemekanazo ziko dunia ya kwanza. Leo hii nimechagua Cambodya na China katika historia .

Tukiachilia mbali siasa na mambo mengi yaliyo izunguka Cambodia, utakutakuwa kitu ambacho uongozi wa Khmer Rouge ulitakakufanya ilikuwa ni kuikomboa Cambodia. Walifikia hatua ya kulazimisha watu kwenda vijijini, na kuwa lazimisha wawe wakulima. Ili kuhakikisha kuwa wanapata tabaka la wakulima walitengeza sera zitakazo wapa watu wapya wenye misingi ya kazi ya ukulima au kwa Kiingereza "New People" through agricultural labor. Wakafanikiwa kufuta pesa na mabenki. Wakafuta maswala ya shule na kulazimisha watoto wa mjini wawe wakulima kijijini. Wale wenye elimu walionekana wameambukizwa fikira potofu hivyo wakauawa na wengine kwenda jela. Lakini kwa ujumla walichokuwa wanajaribu kufanya ilikuwa ni kuikomboa nchi wakiamini kuwa kilimo tu ndio njia pekee. Sishangai kuona jinsi gani walishindwa. Lakini kitu nachokistukia ni kwamba mpaka kwenye blogu zetu nakutana mara nyingine na hoja ambazo zinaonyesha kuwa kuna watu bado wanaamini kabisa katika hoja ambazo zina fanana fanana na Khmer Rouge. Nadhani tunakumbuka hata maswala ya vijiji vya ujamaa. Sasa wakati tunajadili kuwa kilimo ndio jibu pekee kama Mzee Luihamu asemavyo tukumbuke basi na baadhi ya mambo yaliyotushindwisha kufanikisha vijiji vya ujamaa . Tukumbuke basi na mambo yaliyoishindwisha Khmer Rouge kuwabakiza watu vijijini . Kwa maana mara nyingi tunawanyoshea watu vidole wakiwa vijiweni mijini bila kukumbuka kuwa kuwapo kwao vijiweni ni matokeo ya tatizo na sio kiini cha tatizo.

Tukienda China, ni vizuri kumkumbuka Mao Tse Tung na kitu chake alichokiita Hatua Kubwa Mbele(The great leap Forward).Yeye aliamini kuwa ilikwenda mbele basi lazima kuingilia maswala ya viwanda kwa nguvu zote. Watu wakalazimishwa kutengeneza chuma majikoni mwao.Chuma ilikuwa ndio ufunguo wa maendeleo.

Posta la propaganda za Mao likikwa mbia ujanja katika kutatua uchumi ni chuma. "Take steel as the key link, leap forward in all fields".








Hatua nzima aliifanyia kazi bila kuwa na ukweli wa mambo ya jinsi gani mambo yafanyike. Hivyo asilimia kubwa ya mambo watu waliolazimishwa kufanya hayakuzaa matunda. Mashamba hayakutosheleza chakula kwa watu. Viwanda havikuweza kuzalisha bidhaa bora. Watu wakafa njaa. Inasemekana katika kipindi hiki hata ndege karibu waishe China kutokana na amri ya kuwaua kwa sababu ya kuamini wanakula mazao. Kutokana na kuua ndege wadudu kibao walizidi kutokana na kukosa maadui wakuwazuia kuzaliwa kwa wingi kupita kiasi. Haya yote huonyesha jinsi gani jambo moja laweza kuzua tatizo jingine kama mipango na utekelezaji wake ni holela.

Sasa kwa nini naongelea mambo yaliyopita? Si ni ukweli kuwa Tanzania sio Cambodia wala China? Jibu ni ndio. Lakini katika kipindi hiki ambacho ni lazima tuende mbele bado kuna mambo mengi yanayoamuliwa na viongozi wetu kienyejienyeji tu.Sasa matokeo yake ni kwamba tuna weza tukajikuta tunaendelea kufanya majaribio(experiments) na maisha ya watu na nchi ilimradi tu kesho inafika.Tukumbuke kuwa bado Tanzania tunahitaji kiongozi mwenye nguvu awezaye kufanya maamuzi kwa faida ya nchi . Lakini naombea kiongozi huyo asiwe kama wa Khmer Rouge au kama Mao ambaye pamoja na mengi kuna mambo mengi alikuwa anayaamua bila kujua athari zake zitakuwa ni nini. Je , unafikiri viongozi wetu wamejifunza kutoka kwa mapungufu ya Viongozi wa Tanzania waliopita? Au ndio mambo ya kutunza statasi quo? Je viongozi wetu wanajifunza jinsi gani nchi kama China ilistukia tatizo na kugeuza mwelekeo?Je tumejifunza kwanini hawakurukia ubeperi kama wa nchi za magharibi kama USA na Uingereza? Je, Kikwete ndio kiongozi wetu atakaye tatua tatizo?

4 KOMENTI a.k.a Maoni. :-(:

luihamu 7:12 am  

Mzee Simon hongera kwa kuweza kutupa picha kamili ya nchi hizo mbili lakini umezungumzia upande mmoja tu,upande wa madhara na si mafanikio,ningependa utupe picha ya mafanikio ya China hadi leo wako wapi.ASANTE.

Mzee Simon turudi nyuma kidogo,Agano la Kale kama unavyosema teknolojia ni muhimu katika maisha ya leo,naomba unijibu swali langu,kipindi cha abrahamu,mussa,jakobo na wengine je walitegemea kilimo au teknolojia?unadhani Mungu alishindwa kugundua teknolojia wakati ule?Mungu alijua kabisa teknolojia itamdhuru mwanadamu na akaamuwa kuto ileta katika akili ya mwanadamu,na ndipo alipo amuwa kutubariki na mashamba,kwanini basi wakati alimuumba Adamu hakumweka mjini bali shambani?Mzee Simon nakuomba usome UFUNUO ndipo utakapo jua siku za mwisho na mifumo ya teknolojia.

Mzee Simon kama kweli teknolojia inamanufaa katika maisha ya mwanadamu nipe mfano unaoweza kutuonyesha ni jinsi gani bara la Afrika linanufaika na teknolojia na tupate mfano ni jinsi gani bara la Afrika linanufaika na kilimo.Kwa hesabu za haraka haraka naomba unitajie nchi tano za Afrika zinazo tengeneza(SOFTCOPY,PROGRAMME,SIMU AU TEKNOLOJIA YOYOTE ILE INAYOTUMIKA UGHAIBUNI).Mzee Simon kama bara la Afrika linaweza kutengeneza vifaa vya teknolojia mimi sina wasiwasi lakini mambo ya kusubiri vifaa vya teknolojia kutoka ughaibuni!la napinga kabisa, nilini tutajivunia KILIMO CHETU?

Anonymous 11:31 am  

Hivi wakulima wa pamba wakiuza pamaba yao, inasafirishwa vipi nje? Kwa kutumia ungo? Au kutumia teknolojia ya kisasa ya usafiri.

Tatizo moja ninaloona katika mjadala huu ni kutoeleweka maana ya neno teknolojia. Mkulima anapotumia trekta, hiyo sio teknolojia? Mkulima anapoweka fedha zake benki, kule benki ili huduma za kibenki ziwe na ufanisi, unakutana na teknolojia.

Agano la kale unasema hakukuwa na teknolojia? Pengine kuna maagano ya kale tofauti.

Kwanza sielewi kwanini kitu kiwe kwenye agano la kale ndio tukione kuwa kina faida. Kwani hiki kitabu kinachoitwa agano la kale ndio kimekuwa kitabu kikuu cha mwanadamu? Historia ya wayahudi na mitume wao ghafla ndio imekuwa kipimo cha mambo yote ya mwanadamu?

Fuatilia historia yetu hasa kwenye ukanda wa bonde la mto Nile, enzi za Meroe, dola za Zimbabwe, Songhai, Ghana, n.k. ndio utaelewa kuwa teknolojia sio jambo geni kwetu.

Kuna watu wanaofikiri kuwa sisi Waafrika hatuna mchango wowote kwenye ulimwengu wa teknolojia wakati sayansi inayotumika katika teknolojia mbalimbali duniani asili yake Afrika.

Kwahiyo hata kama kwenye hilo agano la kale (na hata jipya) hakuna teknolojia, mimi hilo halitanisumbua maana kwangu mimi hilo agano la kale ni kitabu tu kama vitabu vingine vya historia, mapokeo, hadithi,n.k.

luihamu 2:29 pm  

Kwanini mimi Ras Luihamu natetea KILIMO?kwanini sikubaliani na teknolojia wakati naitumia kila siku?Naomba tujiulize mwanzo wa utumwa ni nini kwanza,tukiweza kujibu swali hili tutajuwa madhara ya teknolojia.Kama Afrika bado inategemea teknlojia kutoka ughaibuni!

luihamu 10:35 am  

teknolojia ya usafirishaji na teknolojia ya ukoloni mambo leo ni vitu viwili tofauti.Tuangalie kwa makini leo hii mashirika makubwa yanaendeshwa kutumia teknolojia,vifaa vinavyotumika kuendesha mashirika mengi vinatoka ughaibuni na tunanunua kwa bei mbaya,wasomi wanaoweza kuvitumia vifaa hivyo ni wachache na wengi wanatoka ughaibuni.kwa mfano benki nyingi zina tuima aina SOFTCOPY kuhifadhi Data,je hizi softcopy zikigoma na nimwisho wa mwezi?tuangalie upande wa simu za mikononi,ndani ya vituo vya internetcafe ni ngono,ngono jamii inajifunza nini?katika misingi yetu ya shule teknolojia haijapewa kipaumbele,kuanzia chekechea ni vigumu ukute mwalimu anafundisha soma la teknolojia lakini kilimo ni mfano hai, kilimo kisichokuwa na madhara yoyote katika mwili wa binadamu.Akili itatendakazi endapo tuna vifaa vya kazi.

Idumu Jumuiya Ya Wanablogu Tanzania


Photo Sharing and Video Hosting at Photobucket

Partner

save mt. Kenya campaign
In partnership with africapoint.com

Taswira BANANGENGE

  © Blogger templates Romantico by Ourblogtemplates.com 2008

Back to TOP